UBORESHAJI WA HUDUMA ZA AFYA UTAHARAKISHA TANZANIA KUFIKIA UCHUMI WA KIPATO CHA KATI

28/12/2018

Morogoro

SEKTA ya afya ina nafasi ya pekee kuiwezesha Tanzania kufikia uchumi wa kipato cha kati kwa haraka endapo wataalamu wa afya watatumia vyema matokeo ya tafiti mbali mbali zinazofanyika katika kupanga, kutekeleza na kutathmini mipango ya maendeleo katika sekta hiyo.

IMG 0005 d4d62Akizungumza leo katika ufunguzi wa semina ya siku mbili ya Utoaji wa Matokeo ya Utafiti wa Kutathmini Upatikanaji wa Huduma za Afya nchini wa Mwaka 2014/15 na Utafiti wa Afya ya Uzazi na Mtoto na Viashiria vya Malaria Tanzania wa Mwaka 2015/16 inayofanyika mkoani Morogoro Katibu Tawala wa mkoa wa Morogoro Clifford Tandari amesema wananchi wanapokuwa na afya bora wanakuwa na uwezo wa kufanya kazi vizuri hivyo kuongeza ufanisi katika uzalishaji mali ambapo matokeo yake ni kuongezeka kwa kiwango wa ukuaji wa uchumi.

“Tunapokuwa na taifa lenye watu wenye afya bora, uwezo wao wa kufanya kazi unakuwa mkubwa, kiwango cha ufanisi kinaongezeka kama ilivyo kwa tija katika uzalishaji na kupelekea kuchagiza kasi ya ukuaji wa uchumi kitu ambacho kinaweza kuifanya Tanzania kufikia uchumi wa kiwango cha kati mapema zaidi” amesema Tandari.

Tandari  amewataka wataalamu kuzingatia vyema matokeo ya tafiti hizo na kuweka mikakati ya kukabiliana na changamoto zilizobainishwa katika tafiti hizo.

“Tafiti zinatuonesha maeneo tunayofanya vizuri na pia maeneo yenye changamoto hivyo hatuna budi tukiwa wataalamu kutumia matokeo haya kuweka mikakati thabiti kukabiliana na changamoto hizo na kuendeleza mafanikio tuliyoyapata” Tandari amesisitiza.

Amesema kuwa mbali ya takwimu zinazotokana na tafiti hizo kuiwezesha Tanzania kujipima katika viashiria vilivyohusika lakini pia inaiwezesha kujilinganisha na nchi nyingine kuona namna inavyopiga hatua katika maeneo mbali mbali.

Malengo makuu ya msingi ya tafiti hizo yalikuwa ni kukusanya takwimu zenye ubora wa hali ya juu kuhusiana na viwango vya uzazi; upendeleo wa jinsia na idadi ya watoto; matumizi ya uzazi wa mpango; afya ya uzazi; afya ya mama na mtoto; hali ya lishe kwa watoto wachanga na akina mama; kiwango cha vifo vya watoto wachanga; umiliki na utumiaji wa vyandarua, magonjwa ya watoto na tiba; na vifo vya akina mama vinavyotokana na matatizo ya uzazi.

Tafiti mbili hizo zilifanywa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) na Ofisi ya Mtakwimu Mkuu wa Serikali, Zanzibar (OCGS) kwa kushikiriana na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Tanzania Bara na Wizara ya Afya, Zanzibar pamoja na Shirika la ICF International la Marekani.

IMG 0019 f4ff6Washiriki wa semina hiyo ambao ni kutoka mikoa ya kanda za Mashariki na Kusini wanajumuisha Waganga Wakuu wa Mikoa, Maafisa Mipango wa Mikoa, Maafisa wa Afya wa Mikoa, Makatibu wa Afya wa Mikoa, Waratibu wa Afya ya Uzazi na Mtoto wa Mikoa, Mameneja wa Takwimu wa Mikoa, Waratibu wa Elimu wa Mikoa, Waratibu wa Madawati ya Jinsia, Maafisa/Waratibu wa Maendeleo ya Jamii na Wawakilishi kutoka Idara ya Mahakama wa Mikoa.  Semina kama hii pia inafanyika Moshi Mkoani Kilimanjaro ikishirikisha mikoa ya Kanda ya Kaskazini.

Mwisho.